MWERA AMAZING BLOG

MWERA AMAZING BLOG

NYUMBA INAYOTUNZA SIRI


NYUMBA inaficha siri kubwa za wanandoa. Ukiwaona mke na mume barabarani wakiongozana na wakati mwingine wakicheka usifikiri wote wanaamani ndani ya mioyo yao.

Makala ya leo inatokana na simulizi niliyosimuliwa na rafiki yangu mmoja anayeishi maeneo ya Temeke, Dar es Salaam.

Ni vizuri nikaweka hapa baadhi ya simulizi hiyo, ili nawe msomaji upate kujua nilichosimuliwa na ikibidi utoe maoni yako.

Soma kisa kwa ufupi:
Rafiki yangu ananisimulia jinsi wanavyoishi maisha ya shida na mkewe kwa zaidi ya miezi miwili sasa. Shida anayosema sio shida ya kukosa matumizi, kula wala sehemu ya kulala.

Shida anayosema ni ugomvi wake na mkewe. Ugomvi wenyewe umesababishwa na yeye (mwanaume) kutoka nje ya ndoa, jambo ambalo mkewe ameligundua na kuamua ‘kumsitishia huduma.’

Anasema, mkewe amegoma kumpikia, kumfulia, kulala naye kitanda kimoja na hata kuzungumza naye. Hiyo ndiyo adhabu aliyoamua kuitoa mwanamke kwa mumewe kwa madai kwamba, huduma hizo hata ‘kimada’ anaweza kumpa. 

Rafiki yangu anadai watazungumza na kucheka na mkewe, labda wanapokuja wageni tu basi! Lakini wakiondoka, mkewe anarudia kukunja ndita.

Kinachomshangaza rafiki yangu huyu ni pale wanapofikiwa na wageni nyumbani kwao. Anasema wanapokuwa pamoja na mkewe hakuna mgeni anayefikiri kama wana matatizo katika ndoa yao.

Anasema yeye na mkewe wanapokuwa na wageni hukaa pamoja, huongea na kucheka utafikiri hawana tatizo. Lakini wakiingia chumbani kwao tu mambo yanarudi kama awali.

Jamaa anashangazawa zaidi  na vitendo vya mkewe anavyovionyesha wakati anapotoka asubuhi kwenda kazini. 

Anasema mkewe akimuona anatoka ndani hutangulia kumsubiri nje na kumuaga kwa bashasha zote “kazi njema mume wangu.” Na mara nyingi anatamka haya mbele za majerani zake.

“Unajua mshkaji wakati mwingine nikiona mke wangu ameniaga kwa bashasha wakati usiku mzima ameninunia nahisi kama ugomvi wetu ndio umekwisha,” anasimulia na kuongeza…

“Na hata jioni nikirudi kutoka kazini, kama nitamkuta nje ananipokea vizuri na hasa kama kutakuwa na watu wengine, lakini tukiingia ndani tu, mziki unakuwa uleule.”

Jamaa anasema amashaomba radhi kwa mkewe kutokana na kosa alilolifanya lakini bado mkwewe ameendelea na msimamo wake wa kumnyima huduma. Anasema huduma inayomuumiza zaidi kuikosa ni kuzungumza na mkewe.

Baada ya rafiki huyu kunipa mksa wake nikamwambia “mkeo ni miongoni mwa wanawake wachache ama waliofundwa wakafundika au waliojifunda wenyewe.”

Akaniuliza kuninyima huduma wewe ndio unaliona jambo zuri la kumsifia?  Nikamwambia hapana. Simsifii kwa hilo. Ninachomsifia ni tabia yake ya kutotangaza matatizo yake na mumewe.

Hata hivyo, nikamwambia kwa kosa ulilofanya ni lazima upewe adhabu, sasa mkeo ameamua kukupa adhabu ndogo tu ya kukunyima huduma kimya kimya ambayo muda si mrefu ataifuta.

Nikamweleza lazima ampongeze mkewe kwa kutotoa siri za ndoa yao. Wapo baadhi ya wanawake na wanaume wasiokuwa na siri na hukisema kwa majerani na marafiki kila kinachofanyika chumbani.

Hekima alizonazo mwanamke huyu zinapaswa kuigwa na wanandoa wengine wake kwa waume. Kila mtu anapaswa kujua kuwa anapotoa siri za ndoa yake pamoja na kumdhalilisha mweziwe pia anajidhalilisha yeye mwenyewe.

Hivi ndivyo nyumba inavyoficha siri. Kama mwanamke huyu angekuwa anapayuka ovyo kwa kumweleza kila mtu matatizo yake na mumewe basi kila mtu mitaani angekuwa anamnyooshea kidole.

Na hata baada ya ugomvi wao kwisha, vidole wangekuwa wananyooshewa wote wawili. Lakini kwa kuamua ‘kufa’ na siri yake moyoni siku utakapomalizika ugomvi hakuna mtu mwingine atakayejua nje ya nyumba yao.

 Hii ndiyo siri ya nyumba ninayotaka msomaji wangu nawe uijue na kuithamini. Ugomvi wako na mumeo au mkeo uishie ndani mwenu, hakuna sababu ya kuwapa faida watu wengine wasio husika na ndoa yenu.

Yanini kuwapa watu faida wakati unajua kama sio kesho basi keshokutwa hali ya amani katika ndoa yenu itarejea kama awali.
Share on Google Plus

About MWERA AMAZING

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment

0 maoni:

Post a Comment