Muungano wa Afrika
umeilaumu jeshi la serikali ya Sudan Kusini na vikosi vya waasi kwa ukiukaji
mkubwa wa haki za binadamu na uhalifu wa kivita.
Uchunguzi wa AU
ulibaini kuwa mapigano yaliyotokea mwezi Disemba mwaka 2013 yalitokana na mzozo
kati ya makabila ya Dinka na Nuer ndani ya kikosi cha kumlinda rais.
Aidha uchunguzi huo
umebaini kuwa vikosi hivyo hasimu viliwachinja watu na kuwalazimisha watu
waliodhaniwa kuwa mahasimu wao kula nyama ya binadamu na kunywa damu yao.
Jopo hilo la uchunguzi
chini ya aliyekuwa rais wa Nigeria Olusegun
Obasanjo limepata majina ya watu
wanaodhaniwa kuwa walioendesha
kampeini hizo za ubakaji wa wanawake na ulaji wa
watu.
Ripoti hiyo
imeorodhesha matukio ya utekaji na udhalilishwaji wa wanawake.
Aidha majina ya watu
waliotekeleza matukio hayo imebainika kuwa ni ya raia ambao hawakuwa
wakishiriki vita vyenyewe.
Matukio mabaya zaidi
yaliripotiwa katika miji ya Juba, Bor, Bentiu na Malakal.
Watu kadhaa
walioshuhudia mwanzo wa vita hivyo mjini Juba wanasema kuwa walilazimishwa
kunywa damu ya watu ambao ndio walikuwa wameuawa.
Makaburi ya halaiki pia
yalifichuliwa katika uchunguzi huo ulioendeshwa tangu mwaka jana jopo hilo la
uchunguzi lilipoundwa.
Maelfu ya watu
wameripotiwa kufariki tangu kuanza kwa vita hivyo yapata miaka miwili.
Watu zaidi ya milioni
mbili wamelazimika kutoroka makwao na kuwa wakimbizi wa ndani kwa ndani.
Jopo hilo limependekeza
watu waliotajwa wafikishwe katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita
iliyoundwa na muungano huo wa Afrika.
Licha ya hofu ya kuwa
maelfu ya watu wa kabila fulani walilengwa na kuuawa jopo hilo linasema kuwa
Hakukuwa na ushahidi uliopatikana wa kuthibitisha kuwa kulifanyika mauaji ya
kimbari.
KUTOKA BBC.
0 maoni:
Post a Comment