Wataalamu wa anga za
juu wa Ulaya kwa ushirikiano na wenzao wa Urusi wamerusha angani chombo cha
anga za juu kitakachofanya utafiti kubaini iwapo kuna uhai sayari ya Mirihi,
kwa Kiingereza Mars.
Chombo hicho kwa jina
ExoMars Trace Gas Orbiter (TGO), kimepaa kutoka Baikonur nchini Kazakhstan saa
09:31 GMT.
Chombo hicho kitafanya
uchunguzi kubaini iwapo gesi ya Methane ambayo imepatikana katika anga ya
sayari hiyo inatokana na shughuli ya kijiolojia au inatokana na viumbe hai.
Mambo yote yakienda
ilivyopangwa, wataalamu wanapanga baadaye kurusha mtambo wa kusafiri juu ya
sayari, kwa kimombo rover, ambao utatumiwa kuchimba chini ya ardhi ya Mars.
Mtambo huo,
utaunganishiwa nchini Uingereza, unaweza kurushwa mwaka 2018 au ukichelewa
mwaka 2020.
Inakadiriwa kwamba
itachukua roketi iliyobeba chombo cha TGO saa 10 ili kujiweka kwenye njia
sahihi ya kuelekea sayari ya Mars.
Safari ya chombo hicho
hadi Mars inatarajiwa kuchukua miezi saba, na sehemu ya chombo kwa jina
Schiaparelli inatarajiwa kutua Mars tarehe 19 Oktoba. Sehemu ya setilaiti ya
chombo hicho itazunguka sayari hiyo ikikusanya maelezo muhimu kuhusu hewa na
gesi zinazopatikana katika sayari hiyo.
Safari ya chombo hicho
inafuatiliwa na wataalamu wa Shirika la Anga za Juu la Ulaya mjini Darmstadt,
Ujerumani.
Mradi huo wa TGO ndio
wa kwanza kabisa kufanywa na Ulaya na Urusi kwa pamoja kuelekea sayari ya Mars,
ambayo ndiyo ya nne kutoka kwenye jua.
Uchunguzi wa awali wa
setilaiti zinazozunguka dunia na rover ya Curiosity ya Marekani umebaini kuwepo
kwa haidrokaboni ingawa za vipimo vya chini sana katika sayari hiyo.
Moja ya mambo
yanayoweza kuwa yanachangia kuwepo kwa gesi hizo ni shughuli za kijiolojia
ndani ya sayari hiyo ambapo maji yanaweza kuwa yanachanganyikana na mawe na
kuzalisha gesi ya haidrojeni ambayo baadaye inageuka na kuwa methane.
Jambo jingine
linaloweza kuwa linasababisha kuwepo kwa gesi hiyo ni kuwepo kwa viumbe hai.
Sehemu kubwa ya gesi ya
methane duniani hutokana na viumbe hai.
kutoka BBC Swahili.
0 maoni:
Post a Comment